Dr Philip Isdory Mpango, Makamu Rais wa Tanzania

Na Rose Mweko,

Kalinzi, Kigoma ,Oktoba 28, 2025

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Philip Mpango amewasili leo katika mji wa Kalinzi, Wilaya ya Kigoma, kwa ajili ya kufunga kampeni za Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika Jimbo la Kigoma Kaskazini, akimuunga mkono mgombea ubunge wa chama hicho, Peter Serukamba.

Dkt. Mpango alipokelewa kwa shangwe na maelfu ya wananchi waliokuwa wamefurika barabarani wakiwa wamebeba mabango na bendera za chama, wakipiga nderemo na vifijo kuashiria mapokezi ya shujaa wa maendeleo.

Akizungumza katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika Uwanja wa Kalinzi, Dkt. Mpango aliwataka wananchi wa Kigoma Kaskazini kuendelea kuiamini CCM kwa kuwa “ndiyo chama pekee chenye dira ya maendeleo na utekelezaji wa vitendo, si maneno.”


"Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeleta mageuzi makubwa katika sekta za barabara, elimu, afya na maji. Ni wajibu wetu kuendeleza kasi hii kwa kumchagua Peter Serukamba, kiongozi mwenye uzoefu, uadilifu na maono ya kweli kwa maendeleo ya Kigoma,” alisema Dkt. Mpango.

Kwa upande wake, Peter Serukamba alimshukuru Makamu wa Rais kwa heshima ya kufika kufunga kampeni zake, akiahidi kuendelea kushirikiana na wananchi kuleta maendeleo katika jimbo hilo, hasa katika kuboresha miundombinu ya barabara, elimu na huduma za kijamii.

Mkutano huo ulipambwa na burudani kutoka kwa vikundi vya ngoma za asili na wanamuziki wa ndani, huku wananchi wakionyesha hamasa kubwa kuelekea uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika hivi karibuni.