Na Rose Mweko, Kigoma

Katika mfumo wa kisiasa wa Tanzania, wanawake wameendelea kupiga hatua kubwa katika uongozi, licha ya changamoto nyingi zinazowakabili. Mgeni Omary, Diwani wa Kata ya Kipampa, na Naibu Meya wa Manispaa ya Kigoma/Ujiji, ni miongoni mwa wanawake shupavu wanaoonyesha uwezo wa wanawake katika uongozi wa kisiasa.

Bi Mgeni Omary Kakolwa alianza uongozi kama mjumbe Serikali ya mtaa wa Lutare 2004-2009 ambapo kwa mafaniko aliyoyapata aliweza kuwa diwani vitimaalum 2010-2020 ambapo baada ya mafanikio ya uongozi katika Nyanja zote hizo Mgeni Omary mwaka 2020 alifanikiwa kugombea udiwani kata ya Kipampa katika kipindi chote cha uongozi wake ameonyesha uthabiti na ujasiri katika utumishi wake huku akiwa taa na kilelezo kwa wanawake wa Kata ya Kipampana Mji wa Kigoma kwa ujumla.



 Aidha Mgeni Amefanikiwa kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo uboreshaji wa huduma za kijamii ambapo ametumia uzoefu wa uongozi kuhimiza ujenzi wa miundombinu bora kama shule, zahanati, na barabara zinazorahisisha usafiri kwa wananchi aidha amekuwa mstari wa mbele kuwahamasisha ushiriki wanawake katika maendeleo kwa kusimamia uanzishwaji wa vikundi vya wanawake kwa lengo la kuwawezesha kiuchumi kupitia mikopo na mafunzo ya ujasiriamali.

Pia Bi Mgeni amekuwa kiongozi mwenye ushirikiano na jamii yake ambapo amejenga mahusiano mazuri kati ya serikali za mitaa na wananchi huku akisisitiza uwazi na uwajibikaji kwa viongozi na watendaji ili kuhakikisha wananchi wanapata haki zao bila kubugudhiwa hii imemfanya kuwa kiongozi anayependwa na wananchi wake.




Kwa upande wa Naibu Meya wa Manispaa ya Kigoma/Ujiji, ameleta mchango mkubwa katika kuimarisha utawala wa kidemokrasia kwa kusimamia vikao vya halmashauri kwa haki na usawa, kuhakikisha sauti ya kila mmoja inasikika, aidha amekuwa mstari wa mbele kupigania maendeleo ya wanawake ambapo amekuwa akihamasisha wanawake wengi kushiriki katika siasa na kujihusisha na shughuli za maendeleo, aidha Bi Mgeni ameweza kuimarisha usafi wa mazingira na huduma za jamii  Kupitia sera zake, amesimamia usimamizi bora wa taka na kuimarisha upatikanaji wa maji safi.

Ushiriki wa wanawake katika siasa una athari chanya kwa jamii kwa njia mbalimbali ikiwemo kuimarisha maendeleo ya jamii kwani wanawake wanapokuwa sehemu ya maamuzi ya kisiasa, wanahakikisha kuwa masuala yanayowahusu wanawake na watoto yanapewa kipaumbele, kama vile elimu, afya, na ustawi wa familia.



Aidha mwanamke anaongeza Kuchochea uwajibikaji na uwazi kwani Tafiti zinaonyesha kuwa wanawake viongozi mara nyingi wanahimiza uwazi na uwajibikaji katika utawala, hali inayosaidia kupunguza rushwa na matumizi mabaya ya madaraka huku wakisaidia kuvunja vikwazo vya kijinsia kwa Wanawake wanaoshiriki katika siasa kwani wanakuwa mfano wa kuigwa kwa kizazi kipya cha wasichana, wakionyesha kuwa uongozi sio wa wanaume pekee.

Hivyo ushiriki wa wanawake katika siasa huleta usawa wa kijinsia na huimarisha uwakilishi wa kijinsia katika vyombo vya maamuzi na kuhakikisha kuwa sauti za wote zinajumuishwa katika sera na maamuzi ya kitaifa na hivyo kuongeza mshikamano wa kijamii kwani wanawake wanasiasa mara nyingi hujikita katika kuimarisha mahusiano ya kijamii na kutatua migogoro kwa njia ya amani, hali inayosaidia kujenga jamii yenye mshikamano na utulivu.



Kumekuwepo na jitihada mbalimbali kimataifa kuhakikisha kunakuwepo na usawa katika uongozi ambapo baadhi ya mikataba ya kutokomeza ubaguzi kimataifa imefikiwa ikiwemo Mkataba wa kutokomeza aina zote za ubaguzi dhidi ya wanawake (CEDAW) – 1979 ulipitishwa na Umoja wa Mataifa (UN) mwaka 1979 na kuanza kutumika mwaka 1981 ndani ya mkataba huo unasisitiza haki za wanawake kushiriki kikamilifu katika maisha ya kisiasa na ya umma (Kifungu cha 7 na 8) aidha unazihimiza nchi wanachama kuchukua hatua za kuhakikisha uwiano wa kijinsia katika ngazi za maamuzi.

Aidha kumekuwepo na maazimio na matamko mengi katika kuhakikisha wanawake wanafikia haki yao katika harakati hizo kumekuwepo na azimio maarufu duniani kama  Azimio la Beijing (Beijing Declaration and Platform for Action) – 1995 ambapo katika azimio hilo lilipitishwa katika Mkutano wa nne wa wanawake wa umoja wa mataifa, miongoni mwa maazimio hayo ni pamoja na kuwa azimio linasisitiza usawa wa kijinsia katika uongozi wa kisiasa na wa kitaasisi aidha inapendekeza sera za kuwezesha uwakilishi wa angalau 50/50 katika siasa na uamuzi wa umma.

Katika mipango mbalimbali ya kimataifa suala la haki sawa kijinsia limepewa kipaumbele ambapo katika Malengo ya Maendeleo Endelevu (Sustainable Development Goals – SDGs) – 2015 lengo namba 5 la SDGs linahimiza usawa wa kijinsia, likilenga kushirikisha wanawake kikamilifu katika uongozi,katika kipengele cha 5.5 kinazitaka nchi kuhakikisha fursa sawa kwa wanawake katika maamuzi ya kisiasa, kiuchumi, na umma.



Mikataba ya kimataifa ya kuhakikisha usawa wa kijinsia katika ngazi za uongozi ni mingi Mkataba wa Maputo (The Maputo Protocol) – 2003 ni mkataba wa umoja wa Afrika (AU) kuhusu haki za wanawake barani Afrika, unasisitiza usawa wa kijinsia katika siasa na maamuzi ya umma (Kifungu cha 9) aidha Mkataba wa SADC juu ya jinsia na maendeleo – 2008 ulipitishwa na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC),ambapo unazitaka nchi wanachama kufanikisha uwakilishi wa 50/50 katika nafasi za uamuzi ifikapo 2030.

Hata hivyo, utekelezaji wa kanuni ya 50/50 bado unakumbwa na changamoto nyingi, ikiwa ni pamoja na mifumo ya kisiasa, mila na desturi, na ukosefu wa sheria za kitaifa zinazounga mkono kikamilifu usawa wa kijinsia.



Sheria za kimataifa kuhusu uwakilishi wa kijinsia wa 50/50 katika ngazi za maamuzi zinatokana na mikataba, maazimio, na makubaliano mbalimbali ya kimataifa kwani hakuna sheria moja ya kimataifa inayotamka moja kwa moja kanuni ya 50/50, lakini kuna nyaraka na makubaliano yanayosisitiza usawa wa kijinsia katika uongozi na maamuzi.

Tanzania ina sheria na sera kadhaa zinazohakikisha usawa wa kijinsia katika ngazi za maamuzi. Ingawa hakuna sheria moja inayotamka moja kwa moja uwiano wa 50/50, kuna nyaraka na sheria zinazosisitiza ushirikishwaji wa wanawake katika uongozi wa kisiasa na maamuzi. Baadhi ya sheria hizo ni pamoja na katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (1977, marekebisho mbalimbali).



 Ibara ya 13(1) na (2) Inasisitiza usawa wa watu wote mbele ya sheria bila ubaguzi wa kijinsia, aidha Ibara ya 66(1)(b) na 78(1)  Inatambua nafasi za viti maalum kwa wanawake katika Bunge ili kuhakikisha ushiriki wao katika maamuzi ya kitaifa huku Ibara ya 9(h) Inalenga kuhakikisha kuwa wanawake wanashiriki kikamilifu katika shughuli za taifa.

Aidha Sheria ya Uchaguzi (1985, marekebisho mbalimbali) Inatoa nafasi kwa wanawake kushiriki kwenye chaguzi za kisiasa kwa kuweka utaratibu wa viti maalum ili kuongeza uwakilishi wao katika Bunge na mabaraza ya mitaa, huku sheria ya Serikali za Mitaa (1982, marekebisho mbalimbali) inasisitiza usawa wa kijinsia katika nafasi za uongozi kwenye serikali za mitaa, pia inahakikisha kuwa wanawake wanashiriki katika mabaraza ya madiwani na maamuzi ya maendeleo ya jamii.

Kwa ujumla, sheria hizi zimechangia kuongezeka kwa idadi ya wanawake katika ngazi za maamuzi nchini Tanzania, lakini bado kuna changamoto za utekelezaji, ikiwa ni pamoja na mifumo ya kijamii na kisiasa inayoweza kuzuia uwiano wa kijinsia katika uongozi.

Pamoja na kuwepo sheria na maazimio mbalimbali ya kuhakikisha wanawake wanapewa kipaumbele katika uongozi bado kuna changamoto wanazokumbana nazo wanawake katika siasa, wanawake katika siasa za Tanzania bado wanakabiliwa na changamoto kadhaa, ikiwa ni pamoja na ufinyu wa fursa za kifedha.



 Wanawake wengi hukosa rasilimali za kifedha za kuendesha kampeni zao na kushindana na wagombea wa kiume wenye mtaji mkubwa hivyo kukata tamaa aidha sababu nyingne ni ukosefu wa usaidizi wa kijamii na familia kwani  majukumu ya kifamilia mara nyingi huwa kikwazo kwa wanawake kushiriki kikamilifu katika siasa.

Aidha vikwazo vya kijamii na kiutamaduni, mila na desturi katika jamii nyingi bado zinapendelea wanaume kushika nafasi za uongozi, hali inayopunguza uungwaji mkono kwa wanawake kwani kumekuwepo na vitendo vya unyanyapaa na vitisho vya kisiasa kwa baadhi ya wanawake kwani hukumbana na matusi, kejeli, na hata vitisho vinavyolenga kuwakatisha tamaa katika safari yao ya kisiasa.



Hivyo basi kumekuwepo na uwakilishi mdogo katika vyama vya siasa licha ya juhudi mbalimbali bado idadi ya wanawake katika vyama vya siasa na nafasi za maamuzi bado ni ndogo ikilinganishwa na wanaume.

Hivyo basi Wanawake kama Mgeni Omary Kakolwa Diwani wa kata ya Kipampa na Naibu Meya wa Kigoma/Ujiji wanaendelea kuwa mfano wa kuigwa kwa wanawake wengine wanaotamani kushiriki katika siasa. Ingawa changamoto bado zipo, mafanikio yao yanaonyesha kuwa kwa kupewa nafasi wanawake wanaweza kuleta mabadiliko chanya katika jamii.

Ni muhimu kwa jamii, serikali, na taasisi za kiraia kuendelea kushinikiza usawa wa kijinsia katika siasa kwa kutoa fursa zaidi kwa wanawake kushiriki na kushikilia nafasi za uongozi kwani demokrasia yenye uwakilishi sawa wa jinsia zote huleta maendeleo jumuishi na kuimarisha ustawi wa jamii kwa ujumla.